Breaking

Post Top Ad

Your Ad Spot

Wednesday, February 22, 2017

USAFIRISHAJI IDADI YA USALAMA NCHINI GAMBIA, HATUA YA KWANZA YA RAIS ADAMA BARROW

Sambamba na kuanza rasmi kazi yake, Rais mpya wa Gambia ametekeleza hatua muhimu katika kuimarisha usalama wa nchi hiyo.
Katika fremu hiyo Rais Adama Barrow ameamuru kutiwa mbaroni kamanda wa zamani wa idara ya usalama wa taifa ya Gambia. Yankuba Badjie, aliyeongoza idara ya usalama wa taifa ya Gambia katika kipindi cha rais wa zamani wa nchi hiyo Yahya Jammeh, na aliyeogopewa sana, ametiwa mbaroni na polisi kwa ajili ya kuhojiwa. Itafahamika kuwa, idara ya usalama wa taifa ya nchi hiyo kilikuwa chombo cha utesaji cha rais huyo wa zamani. Malalamiko ya kutaka kuachiliwa huru shakhsia wa kisiasa na kutoheshimiwa haki za binaadamu, ni miongoni mwa mambo yaliyokuwa yakilalamikiwa sana na wapinzani wa Gambia na hata asasi za kimataifa katika uwanja huo.
Yahya Jammeh, rais wa zamani wa Gambia
Yahya Jammeh aliyetawala Gambia kwa miaka 22, anatuhumiwa kuwakandamiza wapizani na kutumia utesaji na ukatili wa kutisha dhidi ya waandamanaji na wanasiasa waliokuwa wakimkosoa. Suala hilo lilishika kasi hasa katika kipindi cha kampeni za uchaguzi wa rais uliopita, ambapo akthari ya viongozi wa vyama mbalimbali vya siasa na wapinzani dhidi ya serikali walitiwa mbaroni nchini. Hata baadhi ya weledi wa mambo waliutaja ushindi wa Adama Barrow kuwa uliotokana na natija ya vitendo hivyo vya serikali iliyopita. Kwa kuwa na idara ya usalama wa taifa yenye nguvu, Jammeh aliweza kuwakandamiza wapinzani na waandamanaji nchini Gambia ambapo alizuia kila aina ya maandamano na mikusanyiko ya wapinzani. Siku chache zilizopita, naibu mkuu wa shirika la kutetea haki za binaadamu la Human Rights Watch anayeshughulikia masuala ya mipango ya shirika hilo alitoa ripoti iliyoeleza kwamba, serikali ya Jammeh ilikuwa ikitumia vitisho na utesaji dhidi ya viongozi wa vyama vya upinzani na kuwanyima haki zao za msingi.
Rais Barrow akiapishwa kuwa rais mpya wa Gambia
Kiasi kwamba wahisani wa kimataifa walitaka kuwekewa vikwazo viongozi wa serikali ya Gambia kutokana na mienendo yao hiyo. Hivi sasa raia wa nchihiyo na ikiwa ni baada ya miezi kadhaa tangu kujiri mgogoro wa baada ya uchaguzi wa tarehe Mosi Disemba mwaka jana, wanataraji kuona mabadiliko katika utendajikazi wa Rais Barrow. Miongoni mwa ahadi alizozitoa Adama Barrow katika kampeni za uchaguzi ni pamoja na kuheshimu haki za raia na kuanzisha anga ya uhuru wa kisiasa nchini humo. Kadhalika rais huyo mpya aliahidi kufanya marekebisho katika idara ya usalama nchini. Inaonekana kuwa katika hatua ya awali ya ahadi zake ameilenga idara ya usalama ili kwa njia hiyo awe ametekeleza moja ya ahadi hizo na wakati huo huo kudhibiti usalama wa ndani ya nchi kwa ajili ya kukabiliana na kila aina ya ukwamishaji mambo na mapinduzi ya kijeshi kutoka kwa askari wanaomuunga mkono Yahya Jammeh.
Jammeh akiondoka Gambia kuelekea uhamishoni
Katika fremu hiyo, Rais Barrow amebadili jina la idara ya usalama wa taifa na kuwa 'Idara ya usalama wa nchi.' Hata kama Jammeh ameondoka nchini Gambia, lakini bado kuna askari wengi wanaomuunga mkono kiongozi huyo wa zamani wa nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika. Barrow anayehesabika kuwa mfanyabiashara mashuhuri wa Gambia, aliahidi pia kwamba ataboresha hali ya uchumi, kuanzisha fursa za kazi na kuvutia wawekezaji nchini. Hii ni kwa kuwa katika kipindi cha utawala wa Jammeh, uchumi wa Gambia uliporomoka kutokana na siasa zake mbovu, hali ambayo ilisababisha pia kuongezeka umasikini na ukosefu wa ajira kwa vijana. Hivi sasa Wagambia wana matumaini kwamba kipindi hiki cha utawala mpya kitafungua anga mpya ya kisiasa na kuboresha hali ya kisiasa nchini humo.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages