Breaking

Post Top Ad

Your Ad Spot

Saturday, February 11, 2017

KUANZA KUONDOKA ASKARI JESHI WA KUDUMISHA AMANI WA UN NCHINI KODIVAA

Licha ya kuendelea ukosefu wa amani huko Kodivaa katika wiki za hivi karibuni, wanajeshi wa kudumisha amani wa kofia bluu wa Umoja wa Mataifa wamesema kuwa wataondoka nchini humo kwa mujibu wa jedwali la muda ulioainishwa.
Bi Aichatou Mindaoudou Mjumbe Maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Kodivaa ametangaza kuwa kikosi cha kulinda amani cha umoja huo huko Kodivaa kitaanza kuondoka nchini kuanzia Februari 15 mwaka huu. Kikosi hicho kilianza shughuli zake nchini humo mwaka 2004 lengo likiwa ni kurejesha huko uthabiti baada ya kupasishwa azimio nambari 1528 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Wanajeshi hao walisalia Kodivaa kwa miaka kadhaa ili kurejesha amani baada ya nchi hiyo kukumbwa na mgogoro wa kisiasa. Kikosi cha kudumisha amani cha Umoja wa Mataifa kilichopo hivi sasa huko Kodivaa kinaundwa na karibu watu elfu sita wakiwemo raia wa kawaida elfu moja. Pamoja na kuwa kuondoka huko Kodivaa kikosi hicho cha UN kunafanyika kwa mujibu wa makubaliano yaliyofikiwa hapo kabla, lakini wanajeshi hao wanajiandaa kuondoka  huku migogoro mikubwa ya kiuchumi na malalamiko ya wananchi kwa mara nyingine tena ikiiathiri nchi hiyo. Hali hiyo imempelekea  Mjumbe Maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa huko Kodivaa Bi Aichatou Mindaoudou kuitolea mwito jamii ya kimataifa kuisaidia Kodivaa kwa kuzingatia hali ya kiusalama inayolegaega ya nchi hiyo iliyosababishwa na uasi wa hivi karibuni wa wanajeshi wa nchi hiyo.
Aichatou Mindaoudou, Mjumbe Maalumu wa Katibu Mkuu wa UN nchini Kodivaa
Itakumbukwa kuwa mwezi uliopita wanajeshi waliokuwa wakiushikilia mji wa Buake huko Kodivaa walianzisha uasi wakiitaka serikali iwaongezee mishahara na marupurupu mengine. Mbali na wanajeshi hao, wafanyakazi wa sekta ya umma, wakiwemo wafanyakazi wa idara ya zima moto, wale waliostaafu na vyama vya ushirika nao vile vile katika wiki za hivi karibuni wamefanya maandamano na migomo wakitaka kuboreshwa hali ya uchumi wa nchi hiyo. Mivutano hiyo inapamba moto huku kukiwa na wasiwasi juu ya uwezekano wa kushtadi malalamiko ya kisiasa na hivyo kuanza tena maandamano ya kisiasa nchini. Kuboreshwa hali ya uchumi, kuongezwa mishahara na kupunguza idadi ya watu wasio na ajira ni baadhi ya ahadi alizotoa Rais Alassane Ouattara wa nchi hiyo wakati wa kampeni za uchaguzi wa rais.
Rais Alassane Ouattara wa Kodivaa
Hali ya kiuchumi ya Kodivaa haijaboreka licha ya kupita miaka kadhaa, bali kutekelezwa baadhi ya sheria, ikiwemo ile inayohusiana na kuongezwa umri wa wastaafu na kuongezwa gharama ya bima kumezidisha zaidi malalamiko ya wananchi.  
Hata kama Kodivaa baada ya kupita miaka kadhaa ya kukabiliwa na migoro imeendesha uchaguzi huru na wa amani wa rais, lakini katika kipindi cha miezi ya hivi karibuni nchi hiyo imeshuhudia maandamano makubwa khususan ya vyama vya upinzani kufuatia kufanyiwa marekebisho baadhi ya vipengee vya katiba. Wapinzani wanaamini kuwa sheria hizo mpya zina lengo la kumuongezea mamlaka Rais Ouattara. 
Ouattara kwa upande wake ametoa hakikisho kwamba atashughulia matakwa yaliyowasilishwa na wananchi. Rais huyo ameendelea kuahidi kwamba atawaongezea wanajeshi mishahara yao na kuwapatia makazi. Inaonekana kuwa, Rais Alassane Ouattara na serikali anayoiongaza wanafanya juhudi kudhibiti migogoro iliyojitokeza nchini. Katika mazingira hayo, kuondoka huko Kodivaa wanajeshi wa kulinda amani wa kofia bluu wa Umoja wa Mataifa pia ambako kutaanza siku kadhaa zijazo kumezidisha utata kuhusu mchakato wa matukio yanayojiri nchi hiyo. Kuendelea mivutano huko Kodivaa pia kumezidisha uwezekano wa kushtadi machafuko na ukosefu wa amani nchini humo.Sababu hiyo imewafanya baadhi ya wachambuzi wa mambo wasisitize kuendelea kubaki huko Kodivaa wanajeshi wa kofia bluu wa Umoja wa Mataifa; hata hivyo uzoefu unaonyesha kuwa  njia zote za kudumisha amani na uthabiti haziishii kwa nafasi ya askari jeshi wa kulinda amani wa umoja huo, bali hatua nyingine pia zinapaswa kuchukuliwa ili kuboresha hali ya usalama nchini humo.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages