Breaking

Post Top Ad

Your Ad Spot

Thursday, February 9, 2017

RAIS MPYA WA SOMALIA AAPISHWA

Waziri Mkuu wa zamani wa Somalia, Mohamed Abdullahi Farmaajo ameshinda katika uchaguzi wa rais uliofanyika jana nchini humo..
Farmaajo alitangazwa mshindi baada ya Hassan Sheikh Mohamud aliyekuwa akitetea kiti hicho kukubali kushindwa katika duru ya pili ya uchaguzi wa rais wa Somalia uliowashirikisha wabunge.
Farmaajo hakuweza kupata thuluthi mbili ya kura zilizohitajika kwa ajili ya kushinda uchaguzi huo baada ya kupata kura 184 mkabala na 97 za mpinzani wake, Hassan Sheikh Mohamud katika duru ya pili ya uchaguzi huo lakini akatangazwa mshindi baada ya rais anayeondoka kujiondoa katika duru ya tatu.
Uchaguzi huo wa rais nchini Somalia ulifanyika Jumatano ya jana ukiwashirikisha wagombea 22 baada ya kuakhirishwa mara kadhaa.  Punde baada ya kutangazwa mshindi, Farmaajo alikula kiapo kama rais mpya wa Somalia. Kwa sasa rais wa Somalia anachaguliwa na wabunge kutokana na hali mbaya ya usalama nchini humo.
Hassan Sheikh Mohamud  ambaye nafasi yake imechukuliwa na Farmaajo
Wabunge wa Somalia kutoka mabunge mawili ya nchi hiyo wamempigia kura rais wakiwa katika kituo cha jeshi la anga huku kukiwa na ulinzi mkali kote katika mji mkuu Mogadishu kutokana na hofu ya magaidi wa Al Shabab  kushambulia na kuvuruga uchaguzi huo.
Kundi hilo la kitakfiri la Al Shabab lilikuwa limetoa taarifa na kuwataka wafuasi wake wawaue wale wote watakaoshiriki katika uchaguzi huo na kwa msingi huo mji wa Mogadishu ulikuwa na ulinzi mkali kuanzia Jumanne. Pamoja na hayo magaidi wa Al Shabaab walitekeleza hujuma katika uwanja wa ndege wa mji huo.
Kwa kuzingatia hali ya hivi sasa ya Somalia, Farmaajo atakabaliwa na changamoto nyingi sana. Hivi sasa Somalia ina matatizo mengi ya kiuchumi na kiusalama na kwa msingi huo Wasomali wengi wanataraji kuwa serikali mpya itazingatia na kulipa kipaumbele suala la kuimarisha jeshi na vikosi vingine vya usalama ili kurejesha uthabiti chini humo.
Weledi wa mambo wanaamini kuwa Kikosi cha Kulinda Amani cha Umoja wa Afrika AMISOM kimeshindwa kurejesha amani Somalia.
Kupunguza mishahara ya wabunge na kuongeza mishahara ya vikosi vya usalama ni kati ya matakwa muhimu ya wananchi ili vikosi hivyo viwe na motisha katika kurejesha amani nchini humo.
Pamoja na hayo, uingiliaji wa madola ya kigeni na hitilafu za ndani ya nchi ni kati ya sababu kuu ambazo zimepelekea utulivu kukosekana Somalia.
Kutokana na umuhimu wake wa kistratijia katika Pembe ya Afrika na Lango Bahari la Babul Mandab ambalo ni njia muhimu ya kupita meli za mafuta na mizigo duniani, Somalia imekuwa ikikodoelwa macho ya tamaa na madola ya kibeberu.
Hali kadhalika mfumo  uliokita mizizi wa kiukoo ni jambo jingine ambalo limepelekea uthabiti kosekana Somalia kwa muda wa karibu miaka 25 sasa. Malumbano ya koo mbali mbali Somalia ni jambo ambalo limepelekea iwe vigumu kupatikana serikali ya mshikamano wa kitaifa nchini.
Mbali na malumbano hayo ya kiukoo, pia kuna hitilafu za kisiasa miongoni mwa wanasiasa na wanaharakati nchini humo.
Baada ya kuanguka serikali ya Siad Barre mwaka 1992,  Somalia ilishuhudia kuibuka na kuenea kwa kasi pote la ukufurushaji la Uwahhabi kutokana na uungaji mkono wa Saudi Arabia. Pote hilo ambalo lina ufahamu usio sahihi wa Uislamu hasa kuwakufurisha wasiokubaliana na itiakdi zao ni sababu nyingine ya matatizo ya sasa ya Somalia kwa kuzingatia kuwa kundi la kigaidi la Al Shabab linafuata itikadi hiyo ya Kiwahhabi.
Ramani ya Somalia
Mbali na tatizo hilo hivi sasa nchini Somalia kuna makundi kadhaa ya wanasiasa wakiwemo wale wa kiliberali wanaofungamana na nchi za Magharibi na wale ambao wanaunga mkono utawla ulioangushwa wa Siad Barre. Wanasiasa wa kiliberali  wanaamini kuwa,  kufuata mfumo na mtindo wa maisha sawa na wa nchi za Magharibi ndio njia pekee ya kuleta umoja wa kitaifa Somalia. Kundi la wanasiasa wanaofadhilisha mfumo uliokuwepo wakati wa Said Barre wanataka mfumo wa kisochialisti nchini humo. Mrengo wa tatu wa kisiasa Somalia ni ule unaofuata utaifa wa Kisomali na unataka maeneo yote yaliyojitangazia uhuru yarejee katika Somalia moja.
Kwa kuzingatia tafauti hizo za kiukoo, kisiasa na kidini zilizopo nchini Somalia, itakuwa changamoto kubwa kuweza kurejesha uthabiti wa kudumu katika nchi hiyo muhimu ya Pembe ya Afrika.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages