Breaking

Post Top Ad

Your Ad Spot

Wednesday, February 22, 2017

HALI MBAYA YA WAKIMBIZI KATIKA BARA LA AFRIKA

Hali ya maisha katika akthari ya nchi za Kiafrika, imesababisha kuongezeka idadi ya wakimbizi katika bara la Afrika. Hii ni katika hali ambayo, Mpango wa Chakula Duniani (WPF) umetahadharisha kuhusu matatizo ya chakula kwa wakimbizi wa bara hilo.
Kwa mujibu wa indhari iliyotolewa na WFP, takribani wakimbizi milioni mbili katika nchi 10 barani Afrika wanakabiliwa na matatizo yaliyosababishwa na uhaba wa chakula, suala ambalo limepelekea kuzuka hali mbaya katika afya ya jamii. Kwa mujibu wa tangazo la asasi hiyo ya kimataifa, idadi ya wakimbizi barani Afrika iliongezeka mwaka 2016 na kufikia milioni tano, ikilinganishwa na wakimbizi milioni 2 na laki sita mwaka 2011. Hii ni katika hali ambayo, licha ya kuongezeka vyanzo vya fedha, lakini misaada ya chakula imepungua na haitoshi kukidhi mahitaji ya chakula ya wakimbizi hao.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, mgao wa misaada ya chakula katika nchi kumi za Kiafrika zikiwemo za Kenya, Cameroon, Chad, Mauritania, Sudan Kusini na Uganda umepungua hadi kufikia asilimia 50.
Kundi la wahajiri
Nchi nyingi za Kiafrika kwa sasa zinakabiliwa na matatizo ya kiuchumi na mizozo ya kisiasa.  Mazingira magumu ya kiuchumi, ukosefu wa ajira na umasikini umetanda katika nchi hizo jambo ambalo limepelekea akthari ya raia wa nchi mbalimbali barani Afrika hususan vijana wahajiri kuelekea barani Ulaya kwa lengo la kutafuta kazi na kuwa na kipato cha kujikimu kimaisha.
Kupita kwenye njia zenye hatari kubwa katika mipaka ya Libya na kusafiri kupitia bahari ya Mediterania kila siku kumewafanya wahajiri wengi wapoteze maisha.
Hata hivyo mwenendo wa juhudi za wahajiri hao ungali unaendelea. Mwenendo huo umezifanya nchi za Ulaya zitiliane saini makubaliano na baadhi ya nchi za Kiafrika kwa ajili ya kuzuia wahajiri hao kuingia barani humo. Katika uwanja huo, makubaliano yaliyotiwa saini hadi sasa bado hayajatekelezwa kivitendo. Harakati za makundi ya kigaidi na kuibuka suala la ukosefu wa usalama na amani ni tatizo jingine linalowakabili wahajiri hao.
Akthari ya maeneo ya Nigeria yanayoshuhudia harakati za kundi la kigaidi la Boko Haram yamewafanya raia wengi kuwa wakimbizi kutokana na kukosekana amani na usalama katika maeneo yao na hivyo kuomba hifadhi katika maeneo salama au kukimbilia nje ya nchi. Hii ni katika hali ambayo, wengi wa wahajiri hao hivi sasa wanakabiliwa na hatari ya kifo kutokana na uhaba mkubwa wa chakula.
Wakimbizi wa Nigeria wakipata chakula cha msaada
Katika upande mwingine, uhamaji huo wa watu umesababisha madhara katika sekta ya kilimo; na kusimama kilimo na kutopandwa mazao kumepelekea kujitokeza uhaba wa chakula kiasi kwamba, ardhi nyingi za kilimo katika maeneo hayo zimekauka. 
Vita vya ndani na vya kieneo ni changamoto nyingine ya eneo hilo. Katika nchi changa zaidi barani Afrika ya Sudan Kusini vita vinaendelea kushuhudiwa katika hali ambayo, njaa inayakabili maeneo mengi ya nchi hiyo. Takwimu zinaonyesha kuwa, watu milioni moja na laki nne wanakabiliwa na hatari ya kifo katika nchi za Nigeria, Somalia na Sudan Kusini.
Kwa mujibu wa Mfuko wa Watoto wa Umoja wa Mataifa UNICEF, ukame katika nchi ya Somalia umewafanya watoto laki moja na 85 elfu wakabiliwe na janga la njaa. Aidha idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka zaidi na kufikia watoto laki mbili na 70 elfu katika miezi ya usoni. Majimui ya mazingira haya yamewafanya wahajiri wanaotafuta chakula, sio tu wasamahe na kuacha mali na vitu vyao bali wengi wao wajikute wakiangukia mikononi mwa magenge ya magendo ya binadamu huku wanawake wakikumbana na vitendo vya kubakwa.
Wahajiri katika bahari ya Mediterranean
Aidha akthari ya watoto walioangukia mikononi mwa magenge hayo ya magendo ya binaadamu wameuzwa kama bidhaa. Utabiri unaonyesha juu ya kuendelea ukame katika akthari ya maeneo hayo ya bara la Afrika. Katika upande mwingine mazingira mabaya ya kisiasa, vita na mashambulio ya kigaidi nayo yanaendelea kushuhudiwa katika akthari ya nchi hizo. Katika mazingira kama haya, ni azma na irada pekee ya jamii ya kimataifa sambamba na kuongezwa harakati za asasi na jumuiya za kieneo kwa ajili ya kudhamini mahitaji ya chakula na vile vile kupigwa jeki juhudi za kuhitimisha vita na migogoro katika akthari ya nchi hizo ndio itakayoweza kuzuia vifo vya mamilioni ya watu barani Afrika.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages