Breaking

Post Top Ad

Your Ad Spot

Saturday, October 28, 2017

MAGHALA YA NYUKLIA YA MAREKANI; CHANZO CHA UKOSEFU WA AMANI DUNIANI

Maghala ya nyuklia ya Marekani; chanzo cha ukosefu wa amani duniani
Makamu wa Rais wa Marekani ameyataja maghala ya silaha za nyuklia za nchi hiyo kuwa suala linalopelekea kuwepo amani duniani.
Akiwa ziarani kukitembelea kituo cha jeshi la anga cha Minot, Mike Pence Makamu wa Rais wa Marekani amesema hakuna nguvu duniani inayopelekea kuwepo amani sawa na maghala ya silaha za nyuklia za Marekani. 
Mike Pence, Makamu wa Rais wa Marekani 
Matamshi hayo yametolewa katika hali ambayo Marekani inatambulika ulimwenguni kama nchi pekee inayotumia silaha za nyuklia vitani. Miaka 70 iliyopita Wamarekani waliishambulia kwa mabomu ya nyuklia miji miwili ya Hiroshima na Nagasaki huko Japan na kusababisha vifo vya  raia wa nchi hiyo zaidi ya laki tatu baada ya kupitia mateso na masaibu chungu nzima. Kabla ya wakati huo, hakukuwa na silaha yoyote ya kivita iliyotengenezwa na binadamu iliyosababisha mauaji ya kutisha kama hayo. Mashambulizi hayo ya nyuklia yalizua hofu kubwa duniani kwa kadiri kwamba kwa mara ya kwanza katika historia, mwanadamu alikumbwa na wasiwasi wa kuangamizwa dunia nzima. 
Sehemu ya mji wa Hiroshima ulivyosambaratishwa na mashambulizi ya nyuklia ya Marekani 
Miaka minne tu baada ya Marekani kufanya mashambulio hayo ya nyuklia huko Japan, Umoja wa Kisovieti ulilifanyia jaribio bomu lake la kwanza la nyuklia na ni baada ya hapo ndipo kukaanza zama za ushindani wa silaha za nyuklia duniani. Ushindani huo mkubwa uliendelea na kuzifanya nchi mbili za Marekani na Urusi ya zamani mwezi Oktoba mwaka 1962 kukaribia kupigana vita vya nyuklia. Wakati huo kama Urusi ya zamani isingezirejesha karibu na Cuba meli zake zilizokuwa zimebeba makombora ya nyuklia, labda Rais wa wakati huo wa Marekani John F. Kennedy  angeamuru kupiganwa vita vya nyuklia; vita ambavyo katika masaa yake ya awali vingeweza kuua kwa uchache watu milioni 400. Marekani pekee hivi sasa imerundika katika maghala yake ya silaha, silaha za nyuklia ambazo zina uwezo wa kuiharibu dunia mara kadhaa. Hata kama Marekani katika miaka 70 iliyopita haijatumia silaha za aina hiyo, lakini imehusika kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja katika kuenea kwa silaha hizo hatari. Dunia sasa inahofia makabiliano ya kinyuklia kati ya Marekani na Korea ya Kaskazini ambayo yanaweza kusababisha maafa makubwa kati ya pande mbili. 
Hasa ikitiliwa maanani kuwa amani ya dunia anayoikusudia Pence haitokani na uadilifu na ridhaa ya jamii, bali inatokana hofu ya Marekani kutekeleza mashambulizi ya nyuklia dhidi ya nchi nyingine. Kuwepo hofu na wasiwasi wa kusambaratika kikamilifu madola makubwa duniani miaka 70 baada ya kumalizika Vita vya Pili vya Dunia kumezuia kuibuka migogoro kati ya madola hayo. Wakati huohuo nchi zilizokuwa zikimiliki nguvu za nyuklia kama Marekani zilihamisha uhasama na mashindano yao ya kijeshi kutoka ndani ya ardhi za nchi hizo na kuyahamishia katika maeneo yaliyobaki nyuma kimaendeleo na yale yaliyokuwa yakistawi huko Asia, Afrika na Amerika ya Latini. Watu wa maeneo hayo walipoteza maisha na kugharimika pakubwa kufuatia vita hivyo baina ya madola makuu duniani. Kwa ibara nyingine ni kuwa, amani iliyoipata Marekani kwa silaha zake za nyuklia na waitifaki wake wa Ulaya haijakuwa na natija nyingine ghairi ya kusababisha vita na umwagaji damu katika maeneo mengine ya dunia

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages